Kila msomi azingatie Ilani ya Elimu ya ‘Jabal Hirah’
Lengo lisiwe stashahada, astashahada, shahada ya msingi, Uzamivu na Uzamili tu pekee.
Je, Msomi wa Viwango vya juu ni aibu kuitwa Ustaadh?
Safari ya kila mwanafunzi wa Kiislamu kutoka nyumbani kwake kwenda shule/Chuo lazima iwe sawa na ile safari ya Mtume, swallallahu alayhi wa sallam,
kutoka nyumbani kwake kwenda pangoni, Jabal Hirah.
Kama ambavyo Mtume aliambiwa “Soma” kwa Jina la Mola wako basi kila
mwanafunzi wa Kiislamu anatakiwa asome hivyo. Mwenyezi Mungu alimpa
changamoto Mtume Wake kwa sura ya mwongozo.
Kwamba kila atakachokisoma akisome kwa ajili ya Mola wake. “Soma kwa
Jina la Mola wako aliyeumba.” Kipande hiki cha aya za Mwanzo za Qur’an
kinabeba maana kamili ya kusoma.
Aya hiyo ina maana kuwa chochote utakachokutana nacho katika kutafuta
elimu kimeumbwa na Mwenyezi Mungu. Hii maana yake, kimsingi, ni kwamba
vile vinavyosomwa ni matokeo ya kazi ya Mwenyezi Mungu.
Kwa ajili ya kutoa changamoto, Mwenyezi Mungu kaanza na baiolojia ya
mwanadamu mwenyewe anayetakiwa kusoma, “Amemuumba mwanadamu kwa pande la
damu.”
Mwenyezi Mungu hakutaka kuanza kwa kumpeleka mbali mja wake anayetafuta
elimu bali kaanza na umbile lake mwenyewe. Aya hii inawasuta wale
waliofanya jitihada za kutenganisha elimu inayoitwa ya dunia na ile ya
dini.
Jitihada hizo mbaya zilikuwa na hila ya kumtenga Mungu na ile inayoitwa
‘elimu dunia’. Kwamba watu wavisome vilivyoumbwa bila kumjua
aliyeviumba. Ulimwengu umezugwa na kuzugika kwamba Mungu atafutwe zaidi
katika imani ya kiroho, na si katika maumbile aliyoyaumba.
Si ukweli wa kuficha kuwa ulimwengu umeachwa kwenye upofu wa kutomuona
Mungu kwa hila iliyofanywa na Wapinzani wa Mungu. Mungu amebaki kama
“dhana tu ya kiroho” ambapo kumwamini au kutomwamini kama yupo ni hiyari
ya nafsi na si hitajio la kiakili.
Profesa wa Baiolojia hamuoni Mungu katika fani aliyosomea bali
anamtafuta rohoni zaidi kwa mawaidha ya Msikitini ya Sheikh ambaye upeo
wake juu ya maumbile si mkubwa kama ule wa Profesa.
Mwenyezi Mungu aliwahi mapema kutaka waja Wake wasome kwa Jina Lake, na
kisha akaweka wazi mapema kuwa Yeye ndiye aliyeumba. Ilani hiyo ya Elimu
iliukusanya mfumo mzima wa elimu ndani ya tauhiid.
Mosi, kulisoma pande la damu sio kusoma Fiqh wala thanawi bali ni kusoma
sayansi ya Baiolojia ambayo, kwa hila za wapinzani wa Mwenyezi Mungu,
imeitwa ‘elimu dunia’ ili eti msomaji wa sayansi hiyo asilihusishe somo
hilo na dini.
Asome tu na kubobea, akikusanya vyeti vya kitaaluma, stashahada,
astashahada, shahada ya msingi, shahada ya uzamili na uzamivu pamoja na
kupewa heshima lukuki za kitaaluma.
Kazi nzuri yenye mshahara mzuri ndiyo lengo la msomi huyu. Gari nzuri ya
kutembelea, nyumba nzuri ya kuishi, maisha mazuri ya kula na kunywa
ndiyo yanayoonesha umuhimu wa jitihada alizozifanya za kutafuta elimu.
Kama hicho ndicho kilele cha jitihada za kutafuta elimu basi akili ya
binadamu itakuwa imeishia pale ilipoishia ya mnyama napo ni pale pa
kutafuta kula na kunywa.
Ilani ya Elimu iliyotolewa Jabal Hira inatupa mtazamo tofauti kabisa na
huo. Mwanafunzi au Msomi wa Kiislamu lazima aizingatie Ilani hii. Kwa
kuizingatia Ilani hii, kila somo linaingia na kufungiwa ndani ya dhana
ya Tauhiid.
Wakati Qur’an ikitoa changamoto ya matumizi ya akili, na ikitoa dondoo
za kisayansi katika aya mbalimbali ili kumkumbusha mwanadamu, msomi
anapaswa kuielekeza akili yake katika fani yake, na kuisoma Qur’an kama
Ilani ya Elimu yake.
Nguvu ya Tauhiid itakayojengeka kwa kuunganisha Aya za Qur’an na fani
mbalimali za elimu itakuwa kubwa mno. Mwenyezi Mungu ataonekana kwenye
Baiolojia, Kemia, Fizikia, Jiografia, Jiolojia, Hisabati na kadhalika.
Imani itakayojengeka hapa itakuwa ni ya yakini, sio ya mashaka-mashaka.
Ibada itakayofanyika kwa msingi wa elimu hii itakuwa ni ibada ya hakika,
sio ya mazoea na ya mkumbo.
Mwanafunzi atakayesoma kwa mtazamo huu hatahitaji kiboko cha kumswaga
aende Msikitini, na moyo hautamruhusu kukwepa Swala. Mwanafunzi
atakayesoma kwa mtazamo huu hatakuwa mtumishi wa tumbo lake, bali
atakuwa Mtumishi wa Mola wake.
Akili ya msomi wa sampuli hii haitaishia kuijua falsafa ya fani yake
bali itasumbuliwa na ishara za Muumba. Dhikiri au kumkumbuka Mwenyezi
Mungu ambako huonekana kama ni utamaduni wa kiroho ndani ya Majumba ya
Ibada nyakati za swala itachukua sehemu kubwa kichwani na moyoni mwa
msomi huyu.
Kila wakati atatawaliwa na wingi wa utukuzo na shukurani kwa Mwenyezi
Mungu kwa kazi aliyoifanya, kuanzia akili inayomwezesha msomi kusoma
kuja neema nyingine. Umbile lake mwenyewe kila siku na kila wakati
litakuwa ishara mpya ya kumuona Muumba wake.
Anapovaa shati na kujitazama kwenye kioo, hatoishia kuona kuwa kapendeza
bali ataona sanaa ya Mwenyezi Mungu katika umbo lake na mara moja
ataisifu na kuitukuza Kazi ya Mola wake.
Msomi huyu hawezi kupitisha sekunde au dakika bila kulitafakari umbile
lake, na umbile la Mbingu na Ardhi. Akijitazama mwenyewe au akiwatazama
wanadamu wenziwe mara moja humuona Muumba wake.
Anapoyatazama macho yake mwenyewe au ya mwenziwe anayetazamana naye
hutanabahi, ni Nani aliyeweka macho haya mawili yanayofanya kazi muhimu
kwa ushirikiano wa ajabu na ubongo!
Kama anasomea sayansi ya macho basi ndio kabisa atatosheka na jicho tu
kumuona Mola wake hata kabla ya kutazama neema nyingine. Macho
anayosomea yatakuwa msingi wa tauhiid, na yatakuwa ishara ya kila siku
ya kumuona Mola wake.
Kama anasomea kinywa basi atatosheka na mfumo wa kinywa kwa jinsi
ulivyopangiliwa meno yenye kazi ya kukata na kutafuna, na atastaajabu,
ni Nani huyu aliyekipangilia kinywa namna hii!
Kinywa anachokisomea na kubobea kwacho kitakuwa msingi wa tauhiid na
ishara ya kila siku ya kumuona Mola wake. Kama anasomea fuvu la kichwa,
basi atajiuliza wakati wote, ni Nani huyu aliyeweka fuvu gumu ili
kuukinga ubongo ambao unahitaji kweli kukingwa?
Kwa nini ubongo umekuwa ndani, fuvu limekuwa nje, hebu ona madhara
yanayotokea pale ubongo unapoathirika? Ni Nani huyu aliyeuwekea kinga
muhimu ubongo? Laiti fuvu la kichwa lingekuwa laini na la
kubonyea-bonyea, ubongo usingelikuwa salama hata kidogo.
Hivyo, kwa kuvuta tafakuri hii pale anaposomea fani yake, msomi wa
mrengo huu, hubakiwa na jawabu la hakika kichwani mwake kuwa yeye na
kile anachosomea ni matokeo ya kazi aliyofanya Mwenyezi Mungu.
Hivyo, fani yake ya fuvu la kichwa inakuwa msingi wa tauhiid. Moja kwa
moja anamuona Mwenyezi Mungu katika elimu yake, na siyo kumtafuta kwenye
mawaidha ya Sheikh.
Anayesomea jiografia husomea mzunguuko wa sayari, na huona umakini usio
wa kawaida ambao tangu ulimwengu ulipoanza miaka dahari, sayari zimekuwa
zikizunguuka kwa kasi bila ajali yoyote!
Kupatikana kwa usiku na mchana na mabadilikon ya majira ni matokeo ya
mzunguuko huo. Msomi wa fani hii atakayezingatia Ilani ya Elimu ya Jabal
Hirah muda wote atasumbuliwa na swali kichwani, ni Nani huyu aliyeumba
mfumo wa sayari na kuuzunguusha kwa usalama ili kuleta mabadiliko ya
nyakati, usiku na mchana na misimu ya masika, kiangazi, kipupwe na
kadhalika?
Ni Nani aliyeumba Bahari yenye manufaa kwa wanadamu, na kitoweo cha
samaki kinachokamilisha lishe yake? Ni Nani aliyeweka ekolojia ya mvuke
wa maji unaoevukia angani kwa upepo wa miti kwa ajili ya kutengeneza
barafu ambayo hatimaye huyeyuka na kuleta mvua ambayo ni muhimu kwa
maisha ya viumbe vyote vya ardhini?
Bila maji, maisha yasingelikuwepo? Ni Nani huyu aliyeweka ekolojia hii
muhimu? Msomi hapa atamuona Mungu kabla ya kwenda Msikitini. Yeye ndiye
atakayemthibitisha Mungu kuliko Sheikh anayeamini kiroho zaidi.
Kumbukumbu ya Mungu itakuwa ya kudumu akilini mwake, na haitakuwa ile ya
wakati wa swala pekee. Msomi wa Jiolojia naye ataitazama milima na
kuona jinsi inavyoisaidia dunia isiyumbishewe na kasi ya mzunguuko wa
dunia.
Bila milima, amani isingelikuwepo. Maisha yangelikuwa ya kutetemeshwa na
kubidukabiduka wakati wote. Lakini vigingi vilivyowekwa kwa sura ya
milima vinafanya kazi muhimu ya kuibakisha ardhi katika utulivu
unaofanya watu waone kama vile hakuna mzunguuko wowote.
Mtu wa kawaida hupata tabu kuelewa pale anapoambiwa dunia inabimbilika
kwa sababu mbona hatubimbiliki. Hii ni hisani kubwa ya Mwenyezi Mungu
ambayo msomi wa jiolojia anapaswa kuiona na kuwafafanulia watu wasiojua
ili kwa pamoja tuungane kumshukuru Mwenyezi Mungu.
Jiografia ni somo la Kiislamu, na si somo la “kizungu”. Kuyasoma
maumbile ya Mwenyezi Mungu kunamwakisi Muumba, hakumwakisi Mzungu.
Ukisoma jiografia unamuona Mungu, sio Mzungu.
Mifano hiyo itoshe kuonesha athari za Ilani ya Elimu ya Jabar Hirah.
Ilani hiyo haimfanyi msomi Muislamu aache kusoma kwa ajili ya Mola wake
na badala yake ajiwekee lengo bandia la kusomea stashahada,
astatashahada, shahada ya msingi, shahada ya uzamili na shahada ya
uzamivu, na baadae kupata kazi nzuri basi!
Badala yake, Ilani hii ndiyo itakayotupatia Makhalifa wa kweli wa
kusimamisha Ufalme wa Mwenyezi Mungu. Mapinduzi ya kiitikadi yatakuja
yenyewe yakiwa ni matokeo ya athari za ilani hii ya Elimu.
Ilani hii ya elimu ndiyo itakayotupatia wasomi halisi wa Kiislamu katika
kila fani. Mjumuiko wa fani hizi ndio unaojenga jamii ya wasomi
wanaoweza kuendesha mambo ya dunia kwa kuzingatia maamrisho ya Mwenyezi
Mungu.
Wimbo wa kusimamisha Uislamu, mwito wa Jihadi vyote haviwezi kupata
matunda bila kutekeleza Ilani hiyo ya Elimu ya Jabal Hirah. Tunaweza
kirahisi kuimba wimbo wa kusimamisha dola ya Kiislamu, na tunaweza
kirahisi kuitisha jihadi lakini mwisho wa siku, wimbo hautachezeka, wala
mwito hautatimia kama hatutapata Jamii ya watu waliosoma kwa Ilani
hiyo.
Tunaposema Uislamu ni itikadi ya kimapinduzi basi maana yake ni kwamba
kila eneo la maisha linahitaji wasomi wa mrengo wa Kiislamu. Huwezi
kujenga Uchumi wa Kiislamu bila kusomesha wachumi kwa Ilani ya Jabal
Hirah.
Tunapozungumzia kusimamisha Uislamu, na tunapozungumzia Jihadi, dira
letu lazima liangaze mbali sana kwamba hatimaye tutakuwa watu wa aina
gani wa kuendesha serikali, na tuna watu wa aina gani wa kupigana
jihadi.
Kwa Uwezo wa Mwenyezi Mungu na kwa msaada wa Malaika kutoka Mbinguni,
Mtume angeliweza kusimamisha Uislamu siku ileile ya kwanza aliyopewa
Wahyi Jabal Hirah.
Au angeliweza kupigana Jihad Maka badala ya kuhamia Madina. Lakini bado
kulikuwa na kazi ya kuijenga jamii, kuwajenga watu wa kupigana Jihadi,
kuwajenga watu wa kusimamisha Uislamu, na kuwajenga watu wa kutawala na
kutumikia Dola ya Kiislamu.
Kwa nini Mtume aliyekuwa na Nguvu za Mwenyezi Mungu nyuma yake na msaada
wa Malaika alihitaji miaka mingi kusimamisha Dola ya Kiislamu? Jihadi
ni faradhi lakini ni matokeo ya jitihada za awali za kujenga jamii ya
Kiislamu.
Kubwa kabisa katika jitihada hizo ni kusomesha watu elimu zote kwa
kuzingatia Ilani ya Jabal Hirah. Tunahitaji diploma, digrii kwa
kuzingatia ilani hiyo. Hapo ndipo dhana ya mapinduzi ya Kiislamu
itakapotimia.
Kwa ujumla, Ilani hiyo ya Elimu ndiyo ya kuwakomboa Waislamu kifikra na
kiitikadi. Itawatoa katika dhana potofu kuwa ‘ukisoma sana’ Chuo Kikuu
hustahili kuitwa Sheikh au Ustaadh!
Itawajengea hali ya kujiamini kuwa uanataaluma hautenganishwi na usheikh
wala uustaadh. Bali uanataaluma sahihi ni mchanganyiko wa yote hayo.
Yeye huyo huyo awe Daktari, yeye huyo awe Profesa, yeye huyo huyo awe
Sheikh na Ustaadh kwa maana ni msomi yuleyule anayesoma kwa Jina la Mola
wake.
Moja ya amali nzuri katika Uislamu ni kutafuta elimu. Katika Qur’ani Tukugu Mwenyezi Mungu ameanza kumhutubu mwanadamu kwa maneno ya “Kusoma”, “Elimu” na “Kitabu.” Hii ni kwa sababu elimu ni njia ya kufikia saada na ukamilifu wa mwanadamu. Mwanadamu kwa kutumia elimu, anaweza kuainisha mustakbali autakao yeye. Mara zote Mtume Mtukufu (saw) na masahaba zake, walikuwa wakihimiza sana kusoma. Katika mwenendo wa Mtume wa Mwenyezi Mungu imenukuliwa kuwa, baada ya vita vya Badr kila mateka ambaye alikuwa akiwafundisha kusoma na kuandika wakazi 10 wa mji wa Madina, alikuwa akiachiliwa huru. Suala hilo ni ushahidi tosha na wa wazi juu ya uzingatiaji mkubwa wa dini ya Kiislamu na Mtume Muhammad (saw) kuhusiana na elimu na utafutaji wake kwa ujumla. Mtukufu huyo alikuwa akiipa umuhimu mkubwa kila aina ya elimu kama vile alivyomtaka mmoja wa masahaba zake kujifunza lugha ya Kisyriac. Mtume Mtukufu (saw) amepokelewa akisema, “Tafuteni elimu hata kama ni kutoka China.” Hadithi hiyo kama zilivyo hadithi nyinginezo, inasisitizia umuhimu wa elimu katika Uislamu. Sisitizo na ushawishi huo, kuhusiana na elimu, ndivyo vimewafanya Waislamu kutilia umuhimu na kufanya juhudi kubwa za kutafua elimu duniani. Mbali na hayo Waislamu walikuwa wakitarjumu kila athari yoyote ya kielimu waliyoipata. Kwa utaratibu huo, licha ya kwamba, Waislamu waliunda mfumo wa mahusiano kati ya tamaduni za Ugiriki, Urumi, Misri, India na nyinginezo, waliweza pia kuibua utamaduni na ustaarabu muhimu katika historia ya mwanadamu, uliokuja kufahamika kwa jina la “Utamaduni na Ustaarabu wa Kiislamu.”
************************************
Kwa mujibu wa mtazamo wa Waislamu, elimu na dini ni vitu viwili
visivyotengana, bali ni vitu vinavyoenda sambamba. Kadhalika taaluma
mbalimbali za kielimu kama vile fizikia, nyota, elimu ya ardhi, elimu ya
tiba, hesabu na mithili ya hizo, zilikuwa zikifundishwa katika vituo
vya kielimu vya Waislamu. Aidha mbali na hayo, Waislamu waliasisi
maktaba kubwa tofauti katika vituo vya kielimu na kidini na hivyo
kuifanya elimu na dini kuwa vitu viwili vinavyohitajiana. Hii ni katika
hali ambayo uelewa finyu wa viongozi wa Kikristo kuhusiana na uhusiano
wa dini na elimu, ulipelekea historia ya Ulaya kugawanyika katika zama
mbili za kipindi cha imani na kipindi cha elimu, huku wakiifanya elimu
kukabiliana na imani. Katika Karne za Kati, mitazamo ya kielimu na
kifalsafa, ilikuwa ikitolewa tu na kanisa na hakuna msomi yeyote
aliyekuwa na haki ya kutoa nadharia yake ya kielimu kinyume na mtazamo
rasmi wa kanisa, kiasi kwamba, nadharia ya kielimu iliyokwenda kinyume
na mtazamo wa kanisa, ilionekana kuwa ni sawa na kukufuru na kumpinga
Mungu. Kwa msingi huo wasomi waliokuwa wakitoa mitazamo iliyopingana na
mitazamo rasmi ya kanisa walikuwa wakifungwa jela, kuhukumiwa kifo au
kuteketezwa motoni.
*************************************
Dini Tukufu ya Kiislamu iwe ni katika maandiko yake au kwa upande wa mwenendo wake wa kihistoria haina mkinzano wowote ule, bali tangu mwanzoni mwa kudhihiri kwake ilitoa amri ya watu kutafuta elimu, kiasi kwamba, sehemu kubwa ya aya na riwaya za kidini imezingatia zaidi suala la elimu na umuhimu wake na kubainisha thamani ya mtu aliye na elimu. Kwa hakika nafasi ya elimu katika Uislamu ni muhimu mno na ina daraja ya faradhi ya kidini. Hii ni kwa sababu hakuna mipaka katika kutafuta elimu. Kwa mtazamo wa Uislamu elimu zote ambazo zina faida kwa mwanadamu, zinapaswa kusomwa na watu. Kuhusiana na hilo Mtukufu Mtume (saw) anasema, “elimu ni zaidi ya kile ambacho kinaweza kuhesabika, basi chukua kile kilicho bora.” Kwa mujibu wa wa riwaya hiyo, Uislamu haukubana elimu katika fani fulani tu, bali umewataka wafuasi wake kujifunza na kutafuta elimu zote ambazo zina manufaa kwa mwanadamu. Kimsingi ni kuwa, Waislamu wanaamini kwamba, kadiri mtu anavyokuwa na elimu kubwa, ndivyo maarifa yake kwa Mwenyezi Mungu yanavyokuwa mengi. Hii ni kwa sababu kwa mujibu wa fikra ya Kiislamu, elimu na dini ni mambo mawili yanayoambatana kikamilifu. Katika Uislamu elimu yenye manufaa imesisitizwa sana. Aidha kwa mtazamo wa Uislamu, elimu haina maana ya elimu ya kidini au elimu ambayo ina manufaa kwa Akhera tu hapana, bali kusudio la elimu yenye manufaa ni elimu ambayo ina manufaa kwa mwanadamu kwa njia moja au nyingine, yawe ni ya kimaada au ya kimaanawi.
*****************************************
Katika aya ya 11 ya Surat al-Mujaadala, Mwenyezi Mungu anaelezea
umuhimu wa elimu na daraja ya juu waliyonayo maulama na wasomi mbele ya
watu wengine kwa kusema: "Mwenyezi Mungu anawainua walio amini miongoni mwenu, na walio pewa ilimu daraja za juu."Neno ‘Darajaat’ yaani daraja, lililotumika katika aya hii na lenye maana 'mutlaki' yaani bila kuainisha kiwango hasa cha daraja hiyo, katika lugha ya Qur'ani linabainisha adhama na ukubwa. Yaani kwa lugha nyingine ni daraja za juu. Katika kufasiri aya hii tukufu, Sahaba Abudhar al-Ghaffari amenukuliwa akisema kwamba, Mtume wa Mwenyezi Mungu alimwambia: Ewe Abudhar, Mwenyezi Mungu, malaika na mitume wake wanampenda Twalibul-ilmi, yaani mtu anayetafuta elimu. Na elimu haipendwi ila na mtu mwenye saada, hivyo ni furaha gani atakayokuwa nayo mtu mwenye kutafuta elimu siku ya Kiama. Na mtu yeyote anayetoka nyumbani kwake kwa ajili ya kujifunza mlango mmoja wa elimu, basi Mwenyezi Mungu atamuandikia malipo kwa kila hatua atakayoipiga sawa na thawabu za mmoja wa mashahidi wa vita vya Badr. Na mtafutaji wa elimu ni kipenzi wa Mwenyezi Mungu na mtu yeyote atakayekuwa na mapenzi na elimu, basi pepo ni mali yake. Na atakuwa katika radhi za Mwenyezi Mungu asubuhi na jioni na hatoondoka duniani isipokuwa atanyweshwa katika Haudh ya Kauthar. Kisha atakula matunda ya peponi na akiwa peponi atakuwa rafiki wa Hadhrati Khidhri (as).” Katika hadithi nyingine Mtume Mtukufu anasema: “Siku ya Kiama, wakati mtu mwenye elimu na mchaji-Mungu watakuwa kwenye Swiratw, yaani njia nyembamba, mchaji-Mungu ataambiwa, aingie peponi na afurahie matunda ya ibada yake aliyoifanya duniani. Na mtu mwenye elimu ataambiwa; bakia hapa na umuombee shufaa mtu au rafiki yeyote umtakaye, kwani kila yeyote utakayemuombea basi dua yako atakubaliwa. Hivyo yule mtu mwenye elimu atasimama katika kisimamo cha Mitume na kuwaombea marafiki na watu wake wa karibu ili wasamehewe dhambi zao. Kwani siku ya Kiama makundi matatu ndiyo yatakayokuwa na hadhi ya kufanya maombezi yaani shufaa, makundi hayo ni Mitume, wasomi na mashahidi.” Mwisho wa hadithi.
*****************************************
Katika hadithi za Ahlubayti wa Mtume (as) pia umesisitizwa umuhimu wa
kutafuta elimu. Mtume (saw) anasema: “Kujifunza elimu ni faradhi kwa
kila Muislamu.” Hatua ya kusisitizwa sana elimu na kufikia daraja ya
ulazima wa kidini, inaonyesha ni kiasi gani Uislamu unavyotilia umuhimu
suala zima la elimu na kupambana na ujinga. Mbali na hayo Mtume anasema:
“Tambueni kuwa, Mwenyezi Mungu anampenda mtu anayetafuta elimu yoyote
ile.” Maneno haya ya Mtukufu Mtume (saw) yanaonyesha kuwa, elimu haina
kiwango wala mpaka bali elimu haiwezi kuwa na mwisho. Kwa ajili hiyo
ikiwa mtu atajifunza elimu kwa kiwango chochote, basi atakuwa katika
radhi za Mwenyezi Mungu Mtukufu, lakini wale wanaofanya juhudi zaidi
katika njia hiyo, kwa hakika watakuwa wenye kupendwa zaidi. Kuhusiana na
suala hilo Sayyid Muhammad Hussein Twabatwabai msomi na mfasiri mkubwa
wa Qur’ani Tukufu anatafsiri aya ya 9 ya Surat Zumarnayosema: “Je
afanyaye ibada wakati wa usiku kwa kusujudu na kusimama na kuogopa
Akhera na kutarajia rehema za Mola wake…. (ni sawa na asiyefanya hayo)?
Sema: Je, wanaweza kuwa sawa wale wanaojua na wale wasiojua?
Wanaotanabahi ni wale wenye akili tu.” Allamah Twabatwabai
anaamini kuwa, katika aya hiyo suala la kuwa na elimu na kutokuwa na
elimu kwa pamoja limetajwa katika namna ya mutlaqi. Lakini madhumuni
yake ni elimu ya kumjua Mwenyezi Mungu, kwa kuwa elimu hiyo ndiyo
inayomfikisha mwanadamu kwenye ukamilifu na ndio uhalisia wa neno
manufaa. Aidha kutokuwa na elimu hiyo kunamsababishia mwanadamu madhara
makubwa. Lakini elimu nyinginezo, ni kama mali na utajiri ambazo manufaa
yake ni kwa ajili ya maisha ya humu duniani na ni zenye kuishia hapa
hapa duniani. Hivyo hadi sasa tuna makundi mawili ya wasomi, msomi
muuminina msomi asiye muumini. Kundi la kwanza ndilo linalopendekezwa
zaidi na ndilo pia lililo bora. Kadhalika Mwenyezi Mungu anasema: “Soma
kwa jina la Mola wako aliyeumba. Amemuumba Mwanadamu katika pande la
damu. Soma na Mola wako ni Mtukufu mno. Ambaye amefunza (kuandika) kwa
kalamu. Amemfunza mwananadamu asilolijua.” Surat Alaq aya ya
1-5. Katika aya hizi kumetajwa daraja na hadhi ya uepo wa mwanadamu.
Daraja bora zaidi ya mwanadamu ni ile ya mtu aliyesoma na kuelimika.
WABILLAHI TAUFIQ