Kila msomi azingatie Ilani ya Elimu ya ‘Jabal Hirah’
Lengo lisiwe stashahada, astashahada, shahada ya msingi, Uzamivu na Uzamili tu pekee.
Je, Msomi wa Viwango vya juu ni aibu kuitwa Ustaadh?
Safari ya kila mwanafunzi wa Kiislamu kutoka nyumbani kwake kwenda shule/Chu
o lazima iwe sawa na ile safari ya Mtume, swallallahu alayhi wa sallam,
kutoka nyumbani kwake kwenda pangoni, Jabal Hirah.
Kama ambavyo Mtume aliambiwa “Soma” kwa Jina la Mola wako basi kila
mwanafunzi wa Kiislamu anatakiwa asome hivyo. Mwenyezi Mungu alimpa
changamoto Mtume Wake kwa sura ya mwongozo.
Kwamba kila atakachokisoma akisome kwa ajili ya Mola wake. “Soma kwa
Jina la Mola wako aliyeumba.” Kipande hiki cha aya za Mwanzo za Qur’an
kinabeba maana kamili ya kusoma.
Aya hiyo ina maana kuwa chochote utakachokutana nacho katika kutafuta
elimu kimeumbwa na Mwenyezi Mungu. Hii maana yake, kimsingi, ni kwamba
vile vinavyosomwa ni matokeo ya kazi ya Mwenyezi Mungu.
Kwa ajili ya kutoa changamoto, Mwenyezi Mungu kaanza na baiolojia ya
mwanadamu mwenyewe anayetakiwa kusoma, “Amemuumba mwanadamu kwa pande la
damu.”
Mwenyezi Mungu hakutaka kuanza kwa kumpeleka mbali mja wake anayetafuta
elimu bali kaanza na umbile lake mwenyewe. Aya hii inawasuta wale
waliofanya jitihada za kutenganisha elimu inayoitwa ya dunia na ile ya
dini.
Jitihada hizo mbaya zilikuwa na hila ya kumtenga Mungu na ile inayoitwa
‘elimu dunia’. Kwamba watu wavisome vilivyoumbwa bila kumjua
aliyeviumba. Ulimwengu umezugwa na kuzugika kwamba Mungu atafutwe zaidi
katika imani ya kiroho, na si katika maumbile aliyoyaumba.
Si ukweli wa kuficha kuwa ulimwengu umeachwa kwenye upofu wa kutomuona
Mungu kwa hila iliyofanywa na Wapinzani wa Mungu. Mungu amebaki kama
“dhana tu ya kiroho” ambapo kumwamini au kutomwamini kama yupo ni hiyari
ya nafsi na si hitajio la kiakili.
Profesa wa Baiolojia hamuoni Mungu katika fani aliyosomea bali
anamtafuta rohoni zaidi kwa mawaidha ya Msikitini ya Sheikh ambaye upeo
wake juu ya maumbile si mkubwa kama ule wa Profesa.
Mwenyezi Mungu aliwahi mapema kutaka waja Wake wasome kwa Jina Lake, na
kisha akaweka wazi mapema kuwa Yeye ndiye aliyeumba. Ilani hiyo ya Elimu
iliukusanya mfumo mzima wa elimu ndani ya tauhiid.
Mosi, kulisoma pande la damu sio kusoma Fiqh wala thanawi bali ni kusoma
sayansi ya Baiolojia ambayo, kwa hila za wapinzani wa Mwenyezi Mungu,
imeitwa ‘elimu dunia’ ili eti msomaji wa sayansi hiyo asilihusishe somo
hilo na dini.
Asome tu na kubobea, akikusanya vyeti vya kitaaluma, stashahada,
astashahada, shahada ya msingi, shahada ya uzamili na uzamivu pamoja na
kupewa heshima lukuki za kitaaluma.
Kazi nzuri yenye mshahara mzuri ndiyo lengo la msomi huyu. Gari nzuri ya
kutembelea, nyumba nzuri ya kuishi, maisha mazuri ya kula na kunywa
ndiyo yanayoonesha umuhimu wa jitihada alizozifanya za kutafuta elimu.
Kama hicho ndicho kilele cha jitihada za kutafuta elimu basi akili ya
binadamu itakuwa imeishia pale ilipoishia ya mnyama napo ni pale pa
kutafuta kula na kunywa.
Ilani ya Elimu iliyotolewa Jabal Hira inatupa mtazamo tofauti kabisa na
huo. Mwanafunzi au Msomi wa Kiislamu lazima aizingatie Ilani hii. Kwa
kuizingatia Ilani hii, kila somo linaingia na kufungiwa ndani ya dhana
ya Tauhiid.
Wakati Qur’an ikitoa changamoto ya matumizi ya akili, na ikitoa dondoo
za kisayansi katika aya mbalimbali ili kumkumbusha mwanadamu, msomi
anapaswa kuielekeza akili yake katika fani yake, na kuisoma Qur’an kama
Ilani ya Elimu yake.
Nguvu ya Tauhiid itakayojengeka kwa kuunganisha Aya za Qur’an na fani
mbalimali za elimu itakuwa kubwa mno. Mwenyezi Mungu ataonekana kwenye
Baiolojia, Kemia, Fizikia, Jiografia, Jiolojia, Hisabati na kadhalika.
Imani itakayojengeka hapa itakuwa ni ya yakini, sio ya mashaka-mashaka.
Ibada itakayofanyika kwa msingi wa elimu hii itakuwa ni ibada ya hakika,
sio ya mazoea na ya mkumbo.
Mwanafunzi atakayesoma kwa mtazamo huu hatahitaji kiboko cha kumswaga
aende Msikitini, na moyo hautamruhusu kukwepa Swala. Mwanafunzi
atakayesoma kwa mtazamo huu hatakuwa mtumishi wa tumbo lake, bali
atakuwa Mtumishi wa Mola wake.
Akili ya msomi wa sampuli hii haitaishia kuijua falsafa ya fani yake
bali itasumbuliwa na ishara za Muumba. Dhikiri au kumkumbuka Mwenyezi
Mungu ambako huonekana kama ni utamaduni wa kiroho ndani ya Majumba ya
Ibada nyakati za swala itachukua sehemu kubwa kichwani na moyoni mwa
msomi huyu.
Kila wakati atatawaliwa na wingi wa utukuzo na shukurani kwa Mwenyezi
Mungu kwa kazi aliyoifanya, kuanzia akili inayomwezesha msomi kusoma
kuja neema nyingine. Umbile lake mwenyewe kila siku na kila wakati
litakuwa ishara mpya ya kumuona Muumba wake.
Anapovaa shati na kujitazama kwenye kioo, hatoishia kuona kuwa kapendeza
bali ataona sanaa ya Mwenyezi Mungu katika umbo lake na mara moja
ataisifu na kuitukuza Kazi ya Mola wake.
Msomi huyu hawezi kupitisha sekunde au dakika bila kulitafakari umbile
lake, na umbile la Mbingu na Ardhi. Akijitazama mwenyewe au akiwatazama
wanadamu wenziwe mara moja humuona Muumba wake.
Anapoyatazama macho yake mwenyewe au ya mwenziwe anayetazamana naye
hutanabahi, ni Nani aliyeweka macho haya mawili yanayofanya kazi muhimu
kwa ushirikiano wa ajabu na ubongo!
Kama anasomea sayansi ya macho basi ndio kabisa atatosheka na jicho tu
kumuona Mola wake hata kabla ya kutazama neema nyingine. Macho
anayosomea yatakuwa msingi wa tauhiid, na yatakuwa ishara ya kila siku
ya kumuona Mola wake.
Kama anasomea kinywa basi atatosheka na mfumo wa kinywa kwa jinsi
ulivyopangiliwa meno yenye kazi ya kukata na kutafuna, na atastaajabu,
ni Nani huyu aliyekipangilia kinywa namna hii!
Kinywa anachokisomea na kubobea kwacho kitakuwa msingi wa tauhiid na
ishara ya kila siku ya kumuona Mola wake. Kama anasomea fuvu la kichwa,
basi atajiuliza wakati wote, ni Nani huyu aliyeweka fuvu gumu ili
kuukinga ubongo ambao unahitaji kweli kukingwa?
Kwa nini ubongo umekuwa ndani, fuvu limekuwa nje, hebu ona madhara
yanayotokea pale ubongo unapoathirika? Ni Nani huyu aliyeuwekea kinga
muhimu ubongo? Laiti fuvu la kichwa lingekuwa laini na la
kubonyea-bonyea, ubongo usingelikuwa salama hata kidogo.
Hivyo, kwa kuvuta tafakuri hii pale anaposomea fani yake, msomi wa
mrengo huu, hubakiwa na jawabu la hakika kichwani mwake kuwa yeye na
kile anachosomea ni matokeo ya kazi aliyofanya Mwenyezi Mungu.
Hivyo, fani yake ya fuvu la kichwa inakuwa msingi wa tauhiid. Moja kwa
moja anamuona Mwenyezi Mungu katika elimu yake, na siyo kumtafuta kwenye
mawaidha ya Sheikh.
Anayesomea jiografia husomea mzunguuko wa sayari, na huona umakini usio
wa kawaida ambao tangu ulimwengu ulipoanza miaka dahari, sayari zimekuwa
zikizunguuka kwa kasi bila ajali yoyote!
Kupatikana kwa usiku na mchana na mabadilikon ya majira ni matokeo ya
mzunguuko huo. Msomi wa fani hii atakayezingatia Ilani ya Elimu ya Jabal
Hirah muda wote atasumbuliwa na swali kichwani, ni Nani huyu aliyeumba
mfumo wa sayari na kuuzunguusha kwa usalama ili kuleta mabadiliko ya
nyakati, usiku na mchana na misimu ya masika, kiangazi, kipupwe na
kadhalika?
Ni Nani aliyeumba Bahari yenye manufaa kwa wanadamu, na kitoweo cha
samaki kinachokamilisha lishe yake? Ni Nani aliyeweka ekolojia ya mvuke
wa maji unaoevukia angani kwa upepo wa miti kwa ajili ya kutengeneza
barafu ambayo hatimaye huyeyuka na kuleta mvua ambayo ni muhimu kwa
maisha ya viumbe vyote vya ardhini?
Bila maji, maisha yasingelikuwepo? Ni Nani huyu aliyeweka ekolojia hii
muhimu? Msomi hapa atamuona Mungu kabla ya kwenda Msikitini. Yeye ndiye
atakayemthibitisha Mungu kuliko Sheikh anayeamini kiroho zaidi.
Kumbukumbu ya Mungu itakuwa ya kudumu akilini mwake, na haitakuwa ile ya
wakati wa swala pekee. Msomi wa Jiolojia naye ataitazama milima na
kuona jinsi inavyoisaidia dunia isiyumbishewe na kasi ya mzunguuko wa
dunia.
Bila milima, amani isingelikuwepo. Maisha yangelikuwa ya kutetemeshwa na
kubidukabiduka wakati wote. Lakini vigingi vilivyowekwa kwa sura ya
milima vinafanya kazi muhimu ya kuibakisha ardhi katika utulivu
unaofanya watu waone kama vile hakuna mzunguuko wowote.
Mtu wa kawaida hupata tabu kuelewa pale anapoambiwa dunia inabimbilika
kwa sababu mbona hatubimbiliki. Hii ni hisani kubwa ya Mwenyezi Mungu
ambayo msomi wa jiolojia anapaswa kuiona na kuwafafanulia watu wasiojua
ili kwa pamoja tuungane kumshukuru Mwenyezi Mungu.
Jiografia ni somo la Kiislamu, na si somo la “kizungu”. Kuyasoma
maumbile ya Mwenyezi Mungu kunamwakisi Muumba, hakumwakisi Mzungu.
Ukisoma jiografia unamuona Mungu, sio Mzungu.
Mifano hiyo itoshe kuonesha athari za Ilani ya Elimu ya Jabar Hirah.
Ilani hiyo haimfanyi msomi Muislamu aache kusoma kwa ajili ya Mola wake
na badala yake ajiwekee lengo bandia la kusomea stashahada,
astatashahada, shahada ya msingi, shahada ya uzamili na shahada ya
uzamivu, na baadae kupata kazi nzuri basi!
Badala yake, Ilani hii ndiyo itakayotupatia Makhalifa wa kweli wa
kusimamisha Ufalme wa Mwenyezi Mungu. Mapinduzi ya kiitikadi yatakuja
yenyewe yakiwa ni matokeo ya athari za ilani hii ya Elimu.
Ilani hii ya elimu ndiyo itakayotupatia wasomi halisi wa Kiislamu katika
kila fani. Mjumuiko wa fani hizi ndio unaojenga jamii ya wasomi
wanaoweza kuendesha mambo ya dunia kwa kuzingatia maamrisho ya Mwenyezi
Mungu.
Wimbo wa kusimamisha Uislamu, mwito wa Jihadi vyote haviwezi kupata
matunda bila kutekeleza Ilani hiyo ya Elimu ya Jabal Hirah. Tunaweza
kirahisi kuimba wimbo wa kusimamisha dola ya Kiislamu, na tunaweza
kirahisi kuitisha jihadi lakini mwisho wa siku, wimbo hautachezeka, wala
mwito hautatimia kama hatutapata Jamii ya watu waliosoma kwa Ilani
hiyo.
Tunaposema Uislamu ni itikadi ya kimapinduzi basi maana yake ni kwamba
kila eneo la maisha linahitaji wasomi wa mrengo wa Kiislamu. Huwezi
kujenga Uchumi wa Kiislamu bila kusomesha wachumi kwa Ilani ya Jabal
Hirah.
Tunapozungumzia kusimamisha Uislamu, na tunapozungumzia Jihadi, dira
letu lazima liangaze mbali sana kwamba hatimaye tutakuwa watu wa aina
gani wa kuendesha serikali, na tuna watu wa aina gani wa kupigana
jihadi.
Kwa Uwezo wa Mwenyezi Mungu na kwa msaada wa Malaika kutoka Mbinguni,
Mtume angeliweza kusimamisha Uislamu siku ileile ya kwanza aliyopewa
Wahyi Jabal Hirah.
Au angeliweza kupigana Jihad Maka badala ya kuhamia Madina. Lakini bado
kulikuwa na kazi ya kuijenga jamii, kuwajenga watu wa kupigana Jihadi,
kuwajenga watu wa kusimamisha Uislamu, na kuwajenga watu wa kutawala na
kutumikia Dola ya Kiislamu.
Kwa nini Mtume aliyekuwa na Nguvu za Mwenyezi Mungu nyuma yake na msaada
wa Malaika alihitaji miaka mingi kusimamisha Dola ya Kiislamu? Jihadi
ni faradhi lakini ni matokeo ya jitihada za awali za kujenga jamii ya
Kiislamu.
Kubwa kabisa katika jitihada hizo ni kusomesha watu elimu zote kwa
kuzingatia Ilani ya Jabal Hirah. Tunahitaji diploma, digrii kwa
kuzingatia ilani hiyo. Hapo ndipo dhana ya mapinduzi ya Kiislamu
itakapotimia.
Kwa ujumla, Ilani hiyo ya Elimu ndiyo ya kuwakomboa Waislamu kifikra na
kiitikadi. Itawatoa katika dhana potofu kuwa ‘ukisoma sana’ Chuo Kikuu
hustahili kuitwa Sheikh au Ustaadh!
Itawajengea hali ya kujiamini kuwa uanataaluma hautenganishwi na usheikh
wala uustaadh. Bali uanataaluma sahihi ni mchanganyiko wa yote hayo.
Yeye huyo huyo awe Daktari, yeye huyo awe Profesa, yeye huyo huyo awe
Sheikh na Ustaadh kwa maana ni msomi yuleyule anayesoma kwa Jina la Mola
wake.